Juma Abdul ni miongoni mwa walinzi wa pembeni wa kutumainiwa kwenye kikosi cha Yanga, ni mchezaji mwenye uzoefu ambaye ameshacheza mechi nyingi kubwa za kitaifa na kimataifa akiwa na klabu yake au timu ya taifa.
Juma ameweka wazi mechi ambayo hatoisahau katika historia yake ya kucheza soka licha ya
kukumbana na mechi nyingi lakini kuna mechi ambayo inabaki katika kumbukumbu zake.
kukumbana na mechi nyingi lakini kuna mechi ambayo inabaki katika kumbukumbu zake.
“Nimecheza mechi nyingi na zote zilikuwa ngumu, lakini mechi siwezi kuisahau ilikuwa dhidi ya Sagrada Esperanca ya Angola tukafanikiwa kupita kwenda hatua ya makundi kwa sababu ilikuwa na mshikemshike kama vita. Ilikuwa imeandaliwa vizuri sana polisi, mashabiki, TFF wote walikuwa kitu kimoja.”
Kesho Jumamosi Yanga itaiwakilisha Tanzania kwenye mechi ya kimataifa katika kombe la shirikisho Afrika itakapokuwa ikicheza dhidi ya Wolaitta Dicha ya Ethiopia kwenye uwanja wa taifa.
Juma Abdul amezungumzia pia mchezo huo pamoja na umuhimu wa mashabiki kuishangilia timu yao inapocheza katika uwanja wa nyumbani.
“Kambi yetu inaendelea vizuri namshukuru Mungu wachezaji wote wanaendelea vizuri baadhi ya wachezaji wenye kadi wamesharuhusiwa wako nyumbani lakini naamini kwa kuongezeka wachezaji wengine ambao walikuwa na majeraha nina hakika tutafanya vizuri katika mchezo Jumamosi.”
“Mechi kubwa kama hizi ni vizuri kuanzia ugenini kwa sababu ukianzia ugenini unaweza kumsoma mpinzani ili ukirudi kwenye uwanja wa nyumbani umalize mechi. Kikubwa ninachoomba kutoka Yanga (wachezaji, benchi la ufundi, uongozi na mashabiki) mechi hii tuifanye kama fainali tupambane hapa nyumbani ili tupate ushindi mzuri.”
“Mashabiki wetu wa Yanga tunawaomba wajitokeze kwa wingi kwenye mechi kwa sababu kuja kwao kwa wingi uwanjani ndio kunaweza kutupa morali sisi wachezaji kwamba watu wole waliopo uwanjani wanataka kitu kutoka kwetu sisi wachezaji tuliopo ndani ya uwanja na kutatufanya tupigane kufa na kupona kutafuta ushindi.”
Source: Shaffih Dauda
Na: Agape Patrick
Email: agape@spoti.co.tz